Mchekecho (Riwaya) - 18+ Utamu



“Jamani, huyu kijana anaitwa Musa. Namtambulisha kwenu. Yeye ni mpangaji mwenzenu hapa,” alisema mama mwenye nyumba akiwa amesimama sanjari na Musa. Mbele ya Musa alisimama baba Shua na mke wake, mama Shua. Binti yao mdogo, Shua alikuwa akichezacheza chini ya miguu ya wazazi wake hao. Baba na mama Shua walitoka kufunga ndoa kama miezi tisa iliyopita. Wakati wanafunga ndoa, mama Shua alikuwa na mimba ya miezi saba tumboni ya mtoto huyo... “Yeye hana mke wala mchumba kwa mujibu wa maelezo yake,” aliongeza mama mwenye nyumba huyo.“Sawa, karibu sana Musa,” baba Shua alimkaribisha kwa furaha ya kuungaunga. Moyoni alimuona Musa ni kijana kama yeye. Sasa kuishi na kijana vile kwenye nyumba moja na yeye alitoka kufunga ndoa alihisi kama ni kujitafutia majaribu yasiyokuwa na ulazima. “Lakini mama siku nyingine tuletee mpangaji mwenye mke. Unajua mpangaji singo kama huyo tatizo linakuja kuwa kwenye zamu za usafi, huwezi kusema afanye usafi. Matokeo yake mke wangu ndiyo atakuwa na kibarua kizito cha kufanya usafi,” alisema baba Shua... “Lakini mume wangu kwenye nyumba nyingine siku hizi, mpangaji kama ni singo anatoa pesa kwa ajili ya kununulia mafagio na vifaa vingine vya kudekia,” alidakia mama Shua. Yeye aliyatafsiri maneno ya kwenye sauti ya mumewe kama ndiyo ujumbe wake halisi lakini hakujua moyoni alikuwa akiwaza kitu kingine kabisa. “Yeah! Yeah! Nitakuwa nikitoa kila mwezi elfu ishirini ya mafagio,” alisema Musa... “Umeme je? Maana umeme hapa ni elfu hamsini kwa mwezi,” alisema mama mwenye nyumba. “Sawa, nitakuwa nikitoa elfu ishirini na tano,” alikubali Musa... “Halafu mbali na umeme, maji kila mwezi ni elfu ishirini,” aliongeza baba Shua. “Hakuna shaka. Nitatoa elfu kumi.” “Kwa hiyo una maana nje ya kodi, kila mwezi utakuwa ukitoa shilingi elfu hamsini na tano?” mama mwenye nyumba aliuliza kwa sauti ya kutaka jibu la haraka... “Ndiyo mama, wala hakuna shida.” Baba Shua aliumia moyoni kutokana na kitendo cha Musa kujifanya ana pesa sana... “Huyu kijana anajifanya anazo. Kila kitu anatoa. Anataka kuniletea majaribu tu hapa,” alisema moyoni... “Mh! Kaka anaonekana ana pesa. Yaani mafagio tu elfu ishirini. Ina maana umeme hata angeambiwa laki moja angesema atatoa nusu yake. Hiyo ishirini ya mafagio itakuwa yangu,” alisema moyoni mama Shua. Musa alihamia hapo usiku wa siku hiyo na kuanza maisha mapya. Yeye alichukua chumba kimoja na sebule, safi kabisa. *** Asubuhi akiwa anapiga mswaki, mama Shua alitokea, akamsalimia... “Za asubuhi shemeji?” “Salama tu shemeji. Umeamkaje wewe, mista na mtoto?” “Hatujambo...hivi kazi unafanyia wapi shemeji?” “Aaa...!” kabla hajamaliza kusema baba Shua akatokea, Musa akatumia hekima, akaacha kusema na kujibalaguza akiwa ndani ya bukta tu, tena tumbo wazi... “Bwana Musa za asubuhi?” baba Shua alimsalimia. “Salama kaka, umeamkaje?” “Salama. Ungekuwa unapigia mswaki ndani bafuni. Hapa nje naona kama itakuwa usumbufu kwako. Mara mtoto wangu Shua atatoka, mara atakuganda na wewe unataka kuwahi kazini.” “Oo! Oke...oke. Sawa! Nimekupata ndugu yangu.” Lakini kutoka moyoni, baba Shua hakupenda jamaa apige mswaki uani huku tumbo linaonekana wakati mke wake anafanya usafi. Aliamini anaweza kujaribiwa. Baba Shua alizama ndani, uani akabaki mama Shua na Musa... “Mimi nafanya kazi kwenye kampuni moja ya simu za mikononi,” alisema Musa kwa sauti ya kawaida... “Ala! Sawa,” alikubali mama Shua. Wiki moja ilikatika tangu Musa ahamie kwenye nyumba hiyo. Siku moja Musa wakati anatoka kwenda kazini alikutana na mama Shua akitoka bafuni kuoga. Alikuwa ndani ya kanga moja tu, aliyoipitisha kifuani kukatizia kwenye nido. Kuona vile Musa, mwili ulimsisimka. Hata walipopishana, Musa hakukubali. Aligeuka kumwangalia huku akitingisha kichwa cha kuashiria kuhamasika naye… “Du! Bonge la mwanamke kumbe. Sijawahi kumwona vizuri kama leo,” alisema moyoni Musa akiondoka zake. Alipofika nje, alisimama kwanza. Akaendelea kumuwaza mama Shua, akataka kurudi akiamini atamkuta ameshajipamba au kuvaa tayari kwa kuondoka. Kweli, Musa alirudi ndani. Akajipitishapitisha kwake, mwishowe akatoka. Akakutana tena na mama Shua akiwa ndani ya gauni refu mpaka chini miguuni lakini likiwa limemchora mwili wake wote na kuonekana vizuri. Waliongozana kutoka nje… “Kumbe shemeji na wewe unafanya kazi?” Musa alimuuliza mama Shua. “Ee! Nipo Jiji.” “Oke. Mzee ameshaondoka?” “Yeye anaondoka saa tatu.” Baba Shua alitoka mbio mpaka nje, akamwangalia mkewe, alishapotea machoni. Akampigia simu… “Upo wapi mama Shua?” “Nakaribia kituoni baba Shua. Vipi, nirudi?” “Hapana. Vipi, huyu kijana ameshaondoka?” aliuliza kwa makusudi baba Shua. Lengo lake lilikuwa kujua kama waliongozana. Baba Shua, ni mwanaume aliyetokea kumpenda sana mkewe. Tangu uchumba wao mpaka ndoa, hajawahi kupunguza mapenzi yake kwake. Kikubwa ni kwamba, mama Shua ameumbika jamani! Kuanzia kiunoni kwenda miguuni alikatika vizuri. Ungeweza kusema alijengeka kwa mfano wa kinu. Kifua chake, licha ya kuwa na mtoto mmoja, hakikuwahi kuchakaa. Kilikuwa kama cha msichana aliyemaliza masomo ya sekondari mwaka jana. Macho ya mama Shua, kama alipaka rangi pembeni yake alitaka mwenyewe, kwani yeye kiasili ni mweupe lakini pembeni ya macho ni mweusi hivyo kumfanya aonekane kama amepaka wanja muda wote. Wanasema wowowo, wengine wana majina yao mbalimbali. Kwa mama Shua wowowo lilikuwepo jamani. Akitembea akiwa amejifunga kanga au akiwa amevaa suruali au sketi achilia mbali gauni. Wowowo lilimpendeza sana na kuvutia wanaume wengi. Tabasamu lake liliweza kumfanya mwanaume ahisi amekutana na yule malkia aliyewahi kushika nafasi ya kwanza kwa uzuri, Cleopatra wa Misri aliyekuwepo kipindi kirefu nyuma. Baba Shua aliujua uzuri wa mke wake kwani mara nyingi, kila wanapokuwa pamoja, wanaume wamekuwa wakimwangalia sana na hivyo kujua kwamba, mke wake ananyendewa na wanaume kibao. “Sijajua kama ameondoka au la!” alisema mama Shua wakati ukweli ni kwamba walikuwa wote. Alijua akisema wapo wote, mume wake asingependa. Baba Shua alikata simu, mama Shua akamgeukia Musa… “Mume wangu alitaka kujua kama umeshaondoka nyumbani,” alisema mama Shua… “Ana shida na mimi?” “Sijajua,” alijibu mama Shua lakini ukweli aliujua. Mbele, karibia na kituo cha daladala, mama Shua alimuaga Musa kwamba anapanda daladala hapo… “Twende nikupe lifti, nipo na gari nimelilaza hapo mbele,” alisema Musa huku macho yake yakitalii kwenye mwili wa mwanamke huyo mrembo… “Mh! Ngumu sana bwana. Wambeya wakiniona itakuwa ishu.” “Kwani mtaa huu una wambeya?” aliuliza Musa. “Utakosa kweli?” aliuliza mama Shua… “Mh! Hatari!” Basi, mama Shua akashika njia kufika kituoni, Musa naye akashika njia kwenda alikolaza gari. Mbele kidogo, mama Shua aligeuka kumwangalia Musa ambaye naye pia aligeuka kumwangalia mama Shua, wakakutana macho. Mama Shua akakimbiza macho yake mbele, Musa yeye aliachia tabasamu pana… “Da! Noma kweli. Amejua nimegeuka kumwangalia. Lakini hakuna noma, hata yeye amegeuka kuniangalia,” alisema moyoni Musa… “Mh! Si atajua niligeuka kwa ajili yake,” alisema moyoni mama Shua. *** Jioni, Musa ndiye aliyetangulia kufika nyumbani. Akafanya utafiti na kubaini kuwa, kwa jirani yake kulikuwa na mtoto Shua na msichana wa kazi tu. Baba Shua na mama Shua walikuwa hawajarudi. Lakini akiwa chumbani kwake anasikiliza muziki sanjari na kuupumzisha mwili kwa kazi za mchana kutwa, mama Shua aliingia. Yeye Musa aliweza kumwona kupitia dirishani kwake, akamchungulia anavyofika mpaka kuzama ndani… “Da! Mpangaji mwenzangu yupo vizuri sana. Jamaa ameibua kifaa cha uhakika,” alisema moyoni Musa. Mama Shua alipobaini kuwa, Musa alisharudi lakini mumewe alikuwa bado alichukua karatasi na kalamu, akaandika namba zake za simu, akamuita msichana wa kazi na kumpa maagizo… “Dada! “Abee.” “Nenda kwa huyo kaka. Mpe hii namba yangu ya simu. Mwambie awasiliane na mimi, kuna utaratibu nataka kumpa kuhusu usafi wa nyumba.” Msichana wa kazi aliipeleka ile karatasi kwa Musa, akagonga mlango kwa dalili za kunyenyekea… “Karibu,” aliitikia Musa kule ndani huku akitoka na kufungua. “Dada amesema nikupe hii karatasi. Ina namba zake za simu.” “Oke, mwambie asante sana eee…” “Sawa. Amesema uwasiliane naye akupangie utaratibu wa usafi,” aliongeza msichana wa kazi huku akiondoka zake. Musa alishtuka kidogo kusikia anatakiwa kuwasiliana na mama Shua ili ampangie utaratibu wa usafi… “Mh! Mbona kuhusu usafi tulishamalizana? Au kuna lingine?” alijiuliza Musa akirudi ndani. Alizisevu zile namba kwenye simu yake kwa jina la Mpangaji. Kisha akamtumia meseji akimwambia… “Nimepata namba, asante sana. Mimi Musa, mpangaji mpya.” Mama Shua alipoipata namba ya Musa, akaachia tabasamu laini sana na kumjibu… “Asante. Nilipenda tu kukupa namba yangu kwa ajili ya mawasiliano kama ikibidi.” “Da!” Musa alishangaa sana. alihisi ameokota dhahabu juu ya mchanga. “Mawasiliano ni muhimu sana. mimi tena jamani!” “Teh! Teh!” mama Shua alijibu kwa kicheko… Basi, Musa na mama Shua waliendelea kuchati weeee! Mpaka giza lilipoanza kuingia ambapo baba Shua alirudi kutoka kazini kwake akiwa amechoka sana… “Huyu kijana mgeni amerudi?” aliuliza baba Shua huku akikaa hata kabla ya salamu kwa mke wake… “Nadhani, sijafuatilia,” alisema mama Shua… “Amesharudi, si saa zile mimi nilikwenda,” alidakia dada wa kazi ambaye alikuwa anapita na shughuli zake… “We dada,” baba Shua alimuita ili amsikie vizuri kutokana na kauli yake kwamba alisharudi na yeye alikwenda kule… “Abe.” “Ulikwenda kufanya nini?” aliuliza baba Shua…” “Nilikuwa napita kwenda nje nikamwona amerudi,” alijibu msichana wa kazi na kuukimbia ukweli. Alijua akisema ukweli atavuruga maana mhusika mwenyewe aliyemtuma alisema hajarudi na hajafuatilia. “Oke, sawa.” Usiku wakiwa wamelala, baba Shua alimwamsha mke wake… “Mama Shua…mama Shua…” “Abee…abee.” “Naomba tuongee kidogo.” “Sawa,” alikubali mama Shua huku akigeuka kulala sawasawa… “Humu ndani kuna mpangaji kama sisi…” “Ndiyo…” “Sasa nataka kusema kuwa, tupo familia mbili tofauti…” “Ni kweli mume wangu…” “Sasa msimamo wangu ni huu. Kila familia ibaki kuwa kivyake. Sitapenda kuona mazoea yoyote kati ya familia yangu na yule bwana, nadhani nimesikika.” “Nimekusikia mume wangu. Lakini ina maana hata salamu nisimpe?” “Salamu mpe. Sitaki mazoea yale ya ndani kabisa, sipendi hata kusikia.” “Nimekuelewa mume wangu.” “Ndiyo hivyo basi.” *** Asubuhi kulikucha, Shua alitoka uani akiwa hajavaa nguo. Musa alikuwa uani wakati huo na mama Shua alikuwa akitoka chumbani kwenda uani… “He! We Shua kwa nini unatembea bila nguo?” mama yake alimjia juu japo Shua hakuwa mtoto mwenye kujitambua… “Ha! Mchumba unanidhalilisha bwana, hujavaa nguo?! Basi sitakuoa,” alisema Musa akimtania mtoto huyo ambaye hajui lolote… “Unaona sasa, unakosa mchumba hivihivi mwanangu?” Musa alikwenda kuoga, akarudi kujiandaa. Mama Shua naye alijiandaa. Kwenye kutoka, baba Shua alisimama nje. Kwa hiyo Musa alipotoka alikuwa kasi kuashiria anawahi. Mama Shua alipotoka yeye, mumewe alimsemesha maneno mengi yaliyomfanya apitishe dakika tano nzima. Alifanya hivyo ili kumpa Musa nafasi ya kufika mbali ili mama Shua akitoka wasiongozane. Mama Shua alipotoka, alikimbia, baba Shua akamuuliza… “Mbona unakimbia? Unamuwahi nani?” “Jamani baba Shua kwani we’ huoni kwamba nimechelewa mume wangu?” “Sasa ndiyo ukimbie? Si utembee kwa haraka tu. Unakimbia kama vile kuna mtu anakusubiri?” “Mh! Baba Shua bwana. Mbona umekuwa hivyo mume wangu?” alihoji mama Shua huku akiangalia simu yake… “Unachati na nani na we unasema umechelewa kazini?” “Baba Shua, sichati na mtu. Nimeangalia tu simu.’’ Mbele ya safari akiwa ameshapotea machoni mwa mume wake, mama Shua alimtumia meseji Musa… “Umeshatimua?” “Niko barabarani tayari. Vipi? Kwema?” “Kwema. Ah! Mista alinipotezea dakika kidogo, ndiyo nafika kituoni.” “Pole sana. Baadaye basi nitachati na wewe.” “Sawa, usijali.” *** Musa alipofika kazini alimsimulia mfanyakazi mwenzake, aitwaye Miayo kuhusu mama Shua na akaomba ushauri… “Musa, huyo mwanamke anakutaka. Hilo liko wazi kabisa. Lakini sasa mwepuke. Unajua mke wa mtu ni sumu inayoua mara moja?” “Ndiyo, lakini sasa Miayo, si anajileta mwenyewe?” “Musa….ulitaka ushauri au ulitaka nikuunge mkono?” “Nilitaka ushauri.” “Ndiyo huo nimekupa. Utajaza mwenyewe.” Waliachana na kila mmoja akaendelea na kazi. Kichwani, Musa aliazimia kutembea na mama Shua. Kwanza alimwona ni saizi yake licha ya kwamba yeye alishapata mtoto mmoja huyo Shua… “Nikishinda mara moja tu si mbaya. Lakini lazima nicheze naye mechi. Mtu anajikomba mwenyewe, mi kosa langu nini sasa?” alijiuliza, akajipa ujasiri. Akiwa kwenye kuwaza hayo, mara meseji ikaingia, Musa akaifungua haraka sana… “Vipi, umekula?” ilitoka kwa mama Shua… “Haya sasa! mambo kama haya ya kuulizana kama nimekula halafu nimwache? Aaa! Wapi! Hata shetani atanicheka,” alisema moyoni Musa. “Ndiyo nataka nitoke nikale, karibu sana,” alijibu Musa... “Kale bwana! Mwili haujengwi kwa simenti wala matofali, unajengwa kwa misosi mbalimbali. Mimi ndiyo natoka kula naingia job sasa.” “Poapoa.” Moyoni mama Shua alijua wazi kwamba, anatengeneza msala kati yake na mumewe. Alijua mumewe akibaini ukaribu wake na mpangaji huyo patachimbika. Tangu afunge ndoa na mumewe huyo haijawahi kutokea wakatibuana kuhusu mapenzi au uaminifu. “Mh! Yaani baba Shua akijua tu, imekula kwangu. Mbona atanitoa roho!” alisema moyoni mama Shua huku akijipanga kwamba, kuanzia siku hiyo aanze kuidhibiti simu yake kwa kiwango cha kimataifa ili mumewe asije akaidaka na kukutana na uozo wake na Musa. *** Ilikuwa saa tisa na nusu, mama Shua alimtumia meseji Musa... “Mimi natoka job now . Wewe je?” “Hata mimi mama. Ndiyo niko nje hapa.” “Kituo wapi?” aliuliza mama Shua... “Mh! Nataka nipite Morocco nikapige kituo pale Makumbusho.” “Nije nikujoini?” “Mh! Utaweza?” “Naweza, kwa nini nisiweze? Kwani kuna kikwazo gani?” “Njoo.” “Poa.” Musa aliendesha gari huku mawazo yake yote yakiwa kwa mwanamke huyo.
Whatsapp +255 758 018 597

Post a Comment

2 Comments

Karibu sana, tuma ujumbe whatsapp +255 758 018 597 kujipatia simulizi zetu

Emoji
(y)
:)
:(
hihi
:-)
:D
=D
:-d
;(
;-(
@-)
:P
:o
:>)
(o)
:p
(p)
:-s
(m)
8-)
:-t
:-b
b-(
:-#
=p~
x-)
(k)