Riwaya - Mapigo Msitukale (Kivita / Kiintelijensia)

 


Riwaya - Mapigo Msitukale Play Store - Kulaya Simulizi App Whatsapp +255 758 018 597 Chau cafe tunamuona Eman Ga Imba aliendelea kunywa kahawa yake polepole kana kwamba hana shughuli nyingine ya kufanya kwa siku hiyo, kichwani akiwa na mawazo mengi sana akipanga na kupangua juu ya maisha yake ya sasa na baadae, alipotahamaki hata kashata alizokuwa akila zilikwisha moyoni akajiuliza kama aliagiza kashata au ameshazila zimekwisha! Hilo nalo likawa jambo jingine ambalo lilikosa jibu kabisa.
“Chausiku!!”
aliita kwa nguvu kana kwamba aliyekuwa anamuita alikuwa umbali wa kilomita kadhaa lakini kumbe wote walikuwa hapo jirani tu.
Watu walishtuka kwa sauti hiyo hata wengine walidiriki kumtupia maneno yasiyostahili
“Samahani waheshimiwa!”
aliomba msamaha.
“Samahani nini mjinga wewe!”
mmoja alitamka kwa hasira
“Wengine tuna BP utatuuwa bure sura ka Sokwe!”
mwingine aliongeza
Eman aliumia sana moyoni kwa tukio lile, akainamia mezani, akatikisa kichwa kisha akasimama kwa hasira na kuelekea eneo la kunawia mikono, akajitazama kwenye kioo, akatabasamu, kisha akageuka na kurudi alipoketi kwanza.
Kabla hajaketi alisikia sauti nyuma yake,
“Umejiona ee? Ka sokwe, tena wa Gombe!” mmoja alimkejeli, wengine wakaangua kicheko cha dharau na kupiga miluzi.
Hasira za dharula zikamrudia Eman, akageuka na kuelekea upande ambao sauti ile imesikika
“Nani aliyesema vile?” aliuliza kwa kung’aka, wakacheka tena
“Ukimuona utamfanya nini? Fala wewe mtoto wa porini!!” mwingine alisema na wengine wakaangua kicheko. Eman alipiga hatua mbili mbele na kumkunja shati yule aliyesema maneno hayo akamuinua kwa nguvu akamrusha chini, huyo akaanguka chini mzimamzima kama gunia, jamaa akanyanyuka kwa hasira na kumvamia Eman, Eman akamdaka na kupiga vichwa vitatu vya nguvu akamsukuma kidogo na kumrushia makonde kama mvua, kijana yule alichanganyikiwa hata hakuweza kujibu mashambulizi alianguka chini mara ya pili.
“Ameua! Ameua! Ameua!” kelele za watu zilijaza mgahawa ule mara watu wakajaa wanataka kumshika Eman. Yule kijana bado alikuwa chini hajitambui kwa kipondo cha ghafla alichokipata. Eman aliruka kutoka aliposimama akatua juu ya meza na kutaka kutoroka kwa kupitia dirishani, watu walimgombania kwa kumshika shatia wengine suruali, masikini Eman shati lake lilichanika vibaya akabaki na fulana ya ndani na kuwaachia shati wananchi wenye hasira, aliruka kupitia dirisha la mgahawa huo na kudondokea kwenye lundo la mawe kwa kutanguliza mkono, alihisi maumivu makali ya mkono lakini alipogeuka aliona watu wale wanakuja pale alipo, akanyanyuka na kutimua mbio
“Huyo huyo! KEman muuaji huyo!!” kelele za wananchi wale zilikuwa kama kichocheo kwa kijana Eman kuongeza spidi. Mara kwa mbele aligongana na pande la mtu na kuangushwa mbali, alinyanyuka na kuanza kukimbia tena, watu walitoka majumbani na kumuunganishia kama kawaida ya wananchi. Mbio ziliendelea na wananchi nao hawakuchoka, alitokea kwenye wigo wa nyumba la! Hapakuwa na njia aliruka na kupanda ukuta kisha akatokea upande wapili na kupanda tena alitua chini kwa miguu yake mikakamavu na kutimua mbio lakini la haula! Alipokuwa akijaribu kuvuka kichaka kidogo katika eneo hilo alijikwaa vibaya na kuanguka chini, mchezo umekwisha. Watu wakamkEman na kuanza kumpiga hata kumuumiza vibaya, Mungu si Athumani polisi waliwahi kumuokoa kutoka kwenye mikono ya watu wenye hasira.
“Tuachie huyo tummalize! Muuaji huyo!” watu walipiga kelele na wengine bado walidiriki kurusha hata mawe ambayo baadhi yaliwapata askari wale. Askari mmoja akafyatua risasi hewani na watu wale wakatawanyika kwa woga wakikimbia uku na huku wengine wakianguka na kukanyagana vibaya. Eman alichukuliwa mpaka kituo kidogo cha polisi akiwa hatamaniki kwa jinsi alivyolowa damu hata fulana yake aliyobaki nayo baada ya kuwaachia shati watu wale haikujulikana kama ni nyeupe au nyekundu, juu ya jicho lake la kushoto jeraha kubwa lilikuwa bado linavuja damu, mkono wake umevimba, kucha ya kidole gumba cha mguu wa kushoto haikujulikana hata imeng’okea wapi. Askari wale walimpiga Tanganyika jeki bila huruma wala kujali kuwa mwenzao ameumia namna ile wallimkokota tena na makofi juu mpaka kituo kidogo cha polisi na kumlundika selo.
Ndani ya chumba kidogo cha selo katika kituo cha polisi cha kijiji wahalifu walijazana mpaka hewa haikutosha kabisa, walichoka na hata wengine kukosa nguvu, kupoteza fahamu kwa kukosa hewa ya kutosha. Eman aliingia kwenye selo hiyo katika hali ile aliyokuwanayo, akakaribishwa na joto na harufu mbaya haja kubwa na ndogo zilizochanganyika, mwanga hafifu uliopita katika kadirisha kadogo kenye ukubwa wa mlango wa banda la njiwa ndio pekee kalikokuwa kanatoa faraja kwa binadamu hawa waliokuwa na makazi ya muda ndani ya chumba hiki, wote walikuwa na sura za kutisha ambazo bila kuuliza utajua kuwa sasa nimeingia kuzimu. (insta - @kulayasimulizi )
Ucku huo ulikuwa mrefu sana kwa Eman, mawazo mengi yalitawala kichwa chake, maumivu makali yaliusumbua mwili wake, alijituliza kimya kwenye moja ya kona za kijichumba hiko huku akisikia kichefuchefu kama mama mjamzito kila mara alitamani kutema mate lakini atatemea wapi watu wamejazana hata wengine wamekaa kwa kupakatana mh! Mawazo yaliendelea kumsonga hata usingizi mwepesi uliokatishwakatishwa kwa nyimbo za kuchukiza za mbu masikioni mwake ulikuja na kuondoka, aliwaza jinsi anavyoishi kwa shida hana baba hana mama, kula yake ya wasiwasi aliona jamii yote haimtaki, dunia imemchukia, ulimwengu unampa adhabu,
“Kwa nini mimi?” alijiuliza uliza moyoni mara kwa mara hata alipokuwa kwenye kibanda chake huko shambani kwao ambako alipitisha maisha yake ya ujana tangu wazazi wake walipofariki yeye akiwa na umri wa miaka kumi na tano, mama yake alikufa kwa kuliwa na simba na baba yake alikufa akiwa anamuokoa mama yake dhidi ya simba hao wenye njaa na uchu wa nyama ya binadamu. Kila aliporudiwa na picha hii alilia sana na kujiona kuwa yeye ni binadamu mwenye mkosi, akuwahi kuwa na kaka wala dada isipokuwa ndugu tu ambao pia hawakuwa na msaada nae kabisa.
“Eman!!!” aligutushwa na sauti kali ya askari iliyotokea kwenye kadirisha ka mlango wa selo hiyo.
“Afande!” aliitikia kwa uchovu na kujaribu kujiinua kutoa alipokuwepo lakini alijikuta anapata kizunguzungu na kuwaangukia wenzake waliokuwa hapo. Alifika mlangoni pale kwa shida mbele yake alimuona msichana mrembo sana kasimama, mrefu wa wastani maji ya kunde, alivalia vizuri suruali yake ya kitambaa nyeusi na blauzi yake nyeupe huku shingoni kafunga skafu yenye mchanganyiko wa rangi, nywele zake fupi zilizokatwa kiumahili na vinyozi wanaojua kazi yao, kiatu chake kirefu kilimfanya aonekane kuwa ni mrembo anayetunzwa na pedeshee fulani. Dada yule alijivuta taratibu mpaka kwenye dirisha lile. Eman alipokea pumzi safi iliyonukia na kuvutia kutoka kwa mrembo huyo, hakuamini anachokiona ni malaika au binadamu, aliduwaa, akapigwa na bumbuwazi, mikono yake ikiwa imeshika nondo mbili zenye kutu alijikuta anaishiwa nguvu. Mrembo yule alishika nondo zile kwa kubana mikono ya Eman akaiangalia sura ya Eman iliyochoka na kukaukiwa na damu..
“Saringo! Naitwa Saringo” alimwambia Eman kwa sauti ya chini
“Hunijui, ila utanijua punde tu” aliendelea “Haujaua ila umeumiza vibaya, sasa unastahili zawadi kwa kazi uliyoifanya bila kujua, na zawadi hiyo utaipata ukimaliza kazi yako” Saringo alishusha pumzi na kumwangalia Eman usoni na kumuona jinsi alivyochanganyikiwa, akaendelea kumwambia mashairi yake yasiyoeleweka kwa mtu mwenye akili timamu, sasa kwa kukunja sura akamwambia Eman “ Lazima ufungwe, uishie jela!” akageuka nakuondoka zake. Eman akazidi kulowa jasho, maswali yasiyo na majibu yalimzunguka tena ‘nilijua malaika mwema kaja kuniokoa kumbe malaika mbaya wa mauti kanitembelea’ alijiwazia na kuanza kulia. Eman hakupata jibu mwanamke yule ni nani, na anataka nini, utata. Asubuhi ile kalandinga liliwachukua mpaka mahakama ya kijiji, jalada la Eman lilikuwa la tatu kuitwa, taratibu akiwa na pingu mikononi aliingizwa katika chumba cha hakimu na kusomewa mashitaka ya kudhuru mwili, alijikuta hana cha kukana isipokuwa kukubali, kesi ikahairishwa mpaka baada ya siku kumi na nne. Walipokuwa wanarudi kwenye kalandinga alimuona binti yuleyule akiwa amesimama katika kundi la watu waliokuja mahakamani hapo, muonekano wake ulikuwa tofauti na wote pale kwani ndiye aliyevaa nadhifu kuliko wote ‘huyu ni nani?’ Eman alijiuliza hakupata jibu, moyoni alimlaani kuliko anavyomlaani shetani walipogongana macho Eman alitema mate chini na kumuonesha kidole cha kati. Mara alijikuta anatandikwa kofi la kisogoni au vijana huita‘mbata’
“Panda juu unatuchelewesha!” sauti kali ya askari ilisikika. Eman na wengine wakapanda na lori lile kuondoka kwa kasi.
*************
“Una mpenzi mzuri sana, mtoto kaumbika kama Malaika, he he he mbona wewe na yeye hamuendani kabisa au wewe ni mchunga ng’ombe wao!”
mmoja wa mahabusu alimuuliza Eman kwa sauti mbaya ya kukwaruza isitoshe inatisha. Eman aligeuka na kumwangalia akatabasamu kwa sura iliyochoka
“Simjui hata anatoka wapi” alimjibu
“Kwangu ni kama shetani tu yule, anataka kuniua, kunifunga, hilo ndilo limemleta hapa” aliendelea kumueleza yule mahabusu.
“Kwa nini aje kukuona asubuhi yote ile? Au kuna uhusiano wowote na kesi yako?” aliendelea kudadisi mahabusu yule, “Sijui chochote! Mbona maswali mengi umempenda? Mfwate basi, mi nshakwambia smjui! Yule ni shetani tu”
Eman alijibu kwa hasira kidogo na mahabusu yule hakuendelea na maswali yake.
Kesi ilitajwa tena baada ya siku kumi na nne, Eman na wenzake wakiwa na pingu mikononi waliingizwa katika chumba maalumu cha mahabusu mahakamani hapo, Eman alisimama karibu na mlango, mara ghafla alipata mshtuko mkubwa, hakuamini alichokiona nje ya jingo hilo, akakaza macho kutazama kwa makini akayafikicha kidogo aone labda alikuwa ndotoni lakini hapana alichokiona ni sahihi na macho hayakumdanganya. Hakutaka kupoteza hata sekunde katika lile alilokuwa analiona lakini bahati mbaya hakuweza kusikia kinachozungumzwa. ‘Yule sio Chausiku?’ alijiuliza moyoni lakini pia hakutaka kuyaamini macho yake.
Chausiku Binti Saidi, msichana mfupi mwenye afya njema kibonge, mmiliki wa mgahawa unaojulikana kwa jina la Chau Café, msichana huyu ambaye amekuwa pamoja na Eman, wamesoma shule moja ya msingi kijijini hapo na kucheza michezo mingi ya utoto pamoja, yeye alifanikiwa kufika japo darasa la saba wakati Eman alifukuzwa shule akiwa darasa la tano kwa kisa cha kumpiga mawe mwalimu wake wa darasa. Maisha yalimwendea kombo Eman lakini Chausiku ndiye alikuwa akimfadhili japo kwa hela ya sigara au kikombe cha Kahawa, watu walikuwa wakimbeza sana Chausiku kwa jinsi alivyoonesha upendo kwa Eman hii ikapelekea Chausiku kutokuwa karibu sana na kijana huyu ambaye japo alikuwa mchafu, mkorofi lakini moyo wake ulituama kwake kama maji yatuliavyo mtungini yasipoguswa. Vijana wengi walipenda kwenda mgahawani kwake japo tu roho zao zisuhuzike kwa kumuona binti huyu, wapo waliomdanganya kwa pesa na vitu mbalimbali lakini msimamo wake thabiti haukumfanya ayumbishwe na vitu vyote hivyo bali aliuacha moyo wake utue kama kipepeo atuavyo katika ua alilolichagua. Chausiku aliumizwa sana na kisa kilichomkuta Eman, alijua kuwa Eman kwa hali aliyonayo asingeweza kupata msaada wowote wa kisheria au utetezi katika kesi yake, alijitahidi kufanya kila awezalo ili tu amsaidie Eman katika hili.
Jalada la Eman liliitwa, polisi walimtoa katika chumba kile akiwa chini ya ulinzi na kupelekwa katika chumba cha mahakama, akiwa anapita katika kikorido kidogo cha jengo hilo alisikia sauti nyembamba tamu ikipenya masikioni mwake, ilikuwa si ya mwingine bali Chausiku ambaye alikuwa akilia kwa machozi mazito “Mwenyezi Mungu akusaidie” ni maneno aliyomwambia, Eman aligeuka kwa kuiba, alifarijika kuona kumbe wapo katika binadamu awa hawa wanaompenda, kidogo alijisikia mtu kati ya watu.
Kesi ya Eman ilikwisha alihukumiwa kifungo cha miaka miwili na miezi sita jela. Waliondolewa mahakamani na Eman alianza kutumikia kifungo chake huko gereza la kilimo Sogera, gereza lenye kazi ngumu, kulima, kupanda, kuvuna, muda wote mkiwa katika matope, maji machafu, mnakula chakula huku mnanyeshewa na mvua, mateso!.
Sogera ni gereza kubwa sana lililoko nje kabisa ya mji wa Mgosola, lilijengwa zamani na wajerumani wakoloni juu ya mlima. Limezungukwa na ukuta usiopungua mita ishirini kwenda juu na chini ya ukuta huo kumepandwa mikonge kuzunguka gereza zima, katika kona zote na katikati ya pande zote kuna vibanda vipatavyo nane juu kabisa vyenye walinzi wawiliwawili kila kimoja wakiwa na silaha kali, juu ya ukuta kumezungushwa waya maalumu ambao una umeme kwa masaa ishirini na nne, doria haziishi nadani ya gereza hili lenye kila aina ya sifa. Eman alifungwa ndani ya gereza hilo, hakuwahi kufikiri hata siku moja kama angefika mahali pale daima alisikia hadithi tu watu wakisimulia na kusifia sifa mbaya za jingo hilo, aliona kuwa sasa ndio amefika mwisho wa maisha yake, jehanum ya duniani, alikata tama ya kuona tena kijiji chake alichokipenda, watu aliyowapenda, michezo aliyoipenda, shamba lake aliloachiwa na wazazi wake, kila kitu kwake aliona kimefika mwisho na kama kuna kitu alichokichukia tangu muda huo ni Saringo msichana mrembo aliyemhakikishia kufungwa na kuozea jela. ‘Shetani huyu! Shetani mkubwa! Aombe nisitoke ila nifie humu, laiti nikitoka namkatakata vipande na nyama nawapa mbwa wale, naapa’ Eman alijiwazia kwa hasira na uchungu. Akiwa bado ameketi kwenye kigodoro kidogo alisikia sauti ya king’ora hakujua kinahashiria nini alipochungulia katika kadirisha ka mlango aliona wafungwa wote wanakimbilia kwenye uwanja mkubwa, mara mlango wake ukafunguliwa (insta - @kulayasimulizi )
“haya mfungwa kwenda kwa wenzio haraka!!” sauti ya askari ilimfanya atoke mbio, alifika na kukaa katika mstari paamoja na wengine. Akasimama askari mmoja katikati akiwa na kipaaza sauti “leo ni sherehe!!!!” alitangaza “tunakaribisha wageni na pia tunapunguza wengine” aliongeza, uwanja ulikuwa kimya sana alisikika yeye peke yake
“wale wote waliofika hapa peponi leo waje mstari wa mbele haraka!”
alitoa amri
Eman na wenzake saba walisogea mbele wakiwa bado na pingu mikononi, wakasimama mbele, hapo waliweza kuona kila kitu kwa vizuri zaidi.
“kwanza napenda kukukaribisheni hapa Sogera, sehemu takatifu ambayo huna budi kuacha ujinga wako!” aliendelea kusema
“Mnaowaona hapa wote ni watoto wazuri wenye roho nzuri wasiopenda ujinga!”
alisema huku akitafuna big G yake, askari huyu mrefu mpana mwenye tambo la kiaskari hasa aliongea maneno haya bila kuonesha tabasamu wala kutikisika, akiwa na bastola yake kiunoni na sare yake ya magereza iliyomkaa vizuri alionekana si wa kuchezea.
“Nyie was*nge! Mliokuja hapa wiki hii, hii ngome ya mjerumani, ukitaka kuishi vizuri fuata amri kumi za hapa ndani, ukiambiwa inama, inama, usilete ubishi kwani waliopo hapa ni binadamu kama wewe wana mahitaji”alisema askari yule.
Eman aliposikia maneno hayo alisisimka na mwili ulikufa ganzi, askari yule aliendelea…
“Usije kujaribu kutoroka, zawadi ya kutoroka ni kama hii mtayoiona sasa!!!” akageuka nyuma akapaza sauti “Afande, lete hao!” mara wafungwa wanne waliletwa wakiwa wamefungwa kamba mikononi wakiburuzwa kama magunia, walijaribu kukukuruka lakini haikusaidia. Pale aliposimama askari yule palikua na jukwaa kubwa lenye kitu kama goli la mpira, lakini juu yake kulikuwa na kitu tofauti, ubao mnene mkubwa wenye tundu la nusu duara lakini katika tundu lile kulikuwa na kitu kilichokamilisha duala lile kiling’aa sana kana kwamba kuna chuma katikati, stailess steel, na upande wa chini wa goli hilo kulikuwa na ubao mwingine kama ule lakini huu kwenye tundu lake haukuwa na kile kitu kama chuma. Mfungwa mmoja aliburuzwa mpaka pale na kufungwa kwa kamba katika goli lile akielezewa chini shingo yake ikiwa imepachikwa kwenye ile nusu duara mwili ukiwa upande wa pili na kichwa upande mwingine, mara kibao kile cha juu kilifyatuka na kuteremka kwa kasi, akiwa bado kapigwa na bumbuazi Eman alihisi kitu kama jiwe la duara kikimgonga miguuni na kuhisi maumivu, alipoangalia chini ni kitu gani hakuamini macho yake, kichwa cha mtu kinachovuja damu mbichi kikiwa kimekatwa kutoka kwa mfungwa yule aliyefungwa pale golini, Eman alichanganyikiwa hajawahi maishani mwake kuona kichwa kisicho na kiwiliwili, akaanza kukimbia.
***************
“KEman huyo!”
amri ilitolewa, askari wawili walianza kumkimbiza, alipigwa ngwala lakini kwa umahiri mkubwa Eman aliruka samasoti na kutua kwa miguu miwili kabla hajakaa sawa alistukia kamba iliyorushwa kwa ustadi ikimfunga shingoni, akageuka na kurusha ngumi iliyompata askari yule sawia shavuni, kabla hajakaa sawa alipigwa teke moja la kifua na kuyumba akaangukia katika mtaro wa maji machafu akatoka kwa haraka alipata pigo lingine maridadi lililompoteza kabisa akaanguka tena, askari wale wakamfunga kamba na kumburuza mpaka uwanjani naye akawekwa pamoja na wale wanaosubiri kunyongwa, akafunikwa nguo nyeusi kichwani asiweze kuona chochote.
“He he he safi sana kijana! Umediriki kufanya kosa ambalo leo litagharimu maisha yako!” askari yule aliyekuwa na kipaza sauti alimwambia Eman
“Mleteni mbele!”
akasogezwa mbele ya lile jukwaa la kunyongea
“Mtoeni kitambaa!”
akatolewa kitambaa
“Mfungueni pingu!”
akafunguliwa pingu na kubaki huru. Askari yule akasema
“umeonesha ujeuri, umempiga askari wangu, sasa utashughulikiwa ili ujue kuwa hapa ni mahali pa pekee”
alimsogelea Eman na kumwangalia usoni
“kwanza umechoka! Mwili na roho! Nani aliyekuleta huku? Leo utajutia ulichowafanyia wananchi huko uraiani!”
alisema yule askari huku amemkazia macho Eman, Eman alimwangalia askari huyu mwenye macho mabaya, mekundu na alikuwa kila akiongea mdomoni mwake kulitoka harufu ya tumbaku na gongo. Askari yule alimzunguka Eman kama mara tatu hivi.
“Cockroach! Fanculo! Caputana!”
alimtukana Eman kwa lugha ambayo hakuielewa. Eman aliona kuwa sasa mwisho wake umefika.
“Aje mwanaume amshughulikie huyu!”
aliita askari yule. Mara akajitokeza pande la mtu, lenye mwili mkubwa, kifua kipana, sura yake ilionesha kila dalili ya kutokuwa na huruma na mtu, lilimsogelea Eman pale alipo, Eman akarudi nyuma kidogo, lile jitu likamsogelea zaidi, Eman alishikwa na hofu ya kifo alipogeuka nyuma akakuta watu tayari wamefanya duara kubwa hamna pa kupenya, alihisi pigo moja la mgongo lililompeleka chini alipojigeuza kuangalia juu aliliona lile jitu likinyanyua mguu kumkanyaga akajiviringisha upande wa pili na jitu lile likakanyaga chini kwa nguvu kishindo ambacho kilitimua vumbi, Eman kwa kutumia nguvu zote alirusha teke lililompata nyuma ya magoti jitu lile likajikuta limepiga magoti, Eman alijinyanyua haraka. Kelele za wafungwa za kumshangilia Eman zilimpa nguvu akiwa bado anawaangalia wanaomshangilia alipigwa roba maridadi ambayo ilimkosesha pumzi, Eman alikukuruka aliporusha mguu wake kwa nguvu kwa nyuma alilipiga hilo jitu kwenye maeneo nyeti, jitu likamuachia Eman na kujishika maeneo,Eman akaanguka chini akanyayuka haraka na kwa kasi ya ajabu aliruka kitu kama tik tak akalipiga usoni kwa migu miwili, nguvu ile ilimfanya jitu asimame wima bila kujua lakufanya, Eman kijana aliyejaliwa wepesi na kusaidiwa na michezo ya sarakasi aliyokuwa akicheza shuleni aliruka hewani na kumpiga mateke ya kifua, jitu lile lilidaka miguu ya Eman kwa ustadi lakini Eman alijikunja kama samaki na kumpiga kichwa usawa wa pua na kumvunja mfupa wa pua, Eman alianguka chini baada ya kuachiwa na lile jitu ambalo wakati huo lilikuwa linavuja damu puani likiwa limeshika pua, Eman alisogea na kurusha makonde mfululizo yaliyokwenda sawia tumboni ambapo jitu lile liliachia uso na kujishika tumboni na Eman alibadili mashambulizi kupeleka usoni, alitumia mtindo huo kama dakika mbili mpaka jitu lile likawa hoi kabisa. Kelele za wafungwa zikazidi kuufunika uwanja wote askari wakaja kumkEman Eman na kumtoa asije akaleta madhara zaidi.
Masikini Eman, hakujua kuwa aliyempiga ndiye mbabe wa gereza hilo, hakuna na haijawahi kutokea mtu akamshinda, wafungwa walimshangilia Eman na tangu hapo akawa na marafiki wengi na kuogopwa na wafungwa wengine.
(insta - @kulayasimulizi )
**************
Maisha yaliendelea gerezani miezi sita ikapita, kazi, mateso, uonevu ndio ilikuwa sera ya maisha yao na Eman akazoea hali hii, kila kukicha hawaishi kupigana na kuumizana kunyang’anyana vyakula na kutaka kuwageuza wenzao, japo Eman hakupenda hali hiyo.
Ilikuwa asubuhi tulivu sana jumapili fulani, watu wengi walikuja kuwatembelea ndugu zao. Eman alikaa kwenye gogo lililopo ndani ya gereza hilo akitafakari hili na lile akimkumbuka huyu na yule. Mara alihisi gogo lile kutikisika alipogeuka alimuona mfungwa mwingine amekaa jirani naye, Eman akamtazama jamaa yule kwa makini sura yake haikuwa ngeni sana lakini hakukumbuka amemuona wapi, alimtazama tena na tena.
“Rafiki!”
mfungwa yule alimuita Eman kwa sauti ya chini, Eman akaigeuka tena kumwangalia vizuri usoni, Eman akaingiwa na hofu kidogo maana mfungwa huyu hajawahi kukutana naye sura yake ya kawaida tu lakini alipotabasamu aligundua kuwa hakuwa na meno, Eman alisogea pembeni kidogo akamuuliza
“wewe ni nani, mbona sijawahi kukuona?”
“Umenisahau?! Wewe ni Eman Ga Imba siyo?”
Eman alishtuka kuona hata jina lake analijua.
“Ndiyo! Mimi ni Eman Ga Imba mwana wa Nkhunulaindo! Nikusaidie nini?”
Eman alijibu na kuuliza kishari kwa maana ndiyo hali aliyoizoea sasa.
“Mimi naitwa Golam wa Golam!”
alijitambulisha kwa Eman, kisha akatoa lile tabasamu lake ambalo lilimfurahisha Eman hata alitamani kucheka, kwa sababu kweli alifanana na Golam ambaye Eman aliwahi kumuona katika filam huko kijijini kwao.
“Safari imewadia!”
Golam alimnong’oneza Eman
“Safari, safari gani?”
Aliuliza kwa mshangao lakini kwa sauti ya chini
“Mimi na wewe tuna safari ya mbali na ngumu sana, safari hii itatugharimu mengi sana lakini mwisho wake tutaishi kama wafalme he he he! Nilikuwa nakungoja, na sasa umefika. Wewe ni Mate ya Simba, kila mnyama atakukimbia, mapori yote yatakuinamia na kukuheshimu, funga mkanda Eman, safari imewadia” Golam aliongea kwa utulivu mkubwa. Eman hakuelewa anachoambiwa wala anachokisikia, aliduwaa tu akitazama upande wapili jinsi pilikapilika za wafungwa na askari zilivyoendelea
“Unat…”
alitaka kumuuliza Golam lakini alipogeuka hakumuona, Golam alishaondoka pale kitambo na Eman hakuweza kujua ameenda wapi! Eman aliona kama katokewa na shetani la kiume, ‘safari, safari gani, kwenda wapi? Lini? Mh!’ hakuweza kupata jibu juu ya maswali hayo, alinyanyuka pale alipoketi na kuvuta hatua chache kuelekea lango kuu la gereza, alichokiona hakukiamini,
‘Saringo!’
alishaangaa, mara aliitwa kuonana na mgeni wake, alikataa kwenda akamwambia afande kuwa hana mgeni, afande akamsisitizia kwa kuwa alishapewa pesa kidogo na Saringo ili afanye makeke, kwa kuwa wafungwa wa aina ya Eman hawakutakiwa kuonana na ndugu ovyo. Alikwenda lakini moyoni mwake hakutaka maishani kuonana na kiumbe huyu mwenye uzuri uliofunika unyama wake.
“Unataka nini tena? Nimeshafungwa! Unataka kuniambia kuwa nitanyongwa, sivyo?”
Eman alimwambia Saringo.
“Eman! Nimekuja kukuomba msamaha, maneno yale sikutegemea kama yatakuwa kweli, wewe hunijui wala mimi sikujui ila nilitumwa kwako na aliyenituma anakuhitaji sasa!”
Saringo aliongea kwa uchungu akimwangalia Eman machoni mwake. Kisha akaingiza mkono kwenye pochi yake akatoa kikaratasi cha rangi ya dhambarau kimekunjwakunjwa akatazama huku na huku akamkabidhi Eman, Eman akakipokea akakificha kwenye nguo ya ndani. Saringo akatoa tabasamu la nguvu kwa Eman, kisha akageuka na kuondoka zake, Eman alibaki anamwangalia akifarijika kuona jinsi mtoto huyu alivyojaaliwa hata upande wa nyuma
‘mashaallah’
alijisemea moyoni, mara alijikuta vurugu kubwa inatokea ndani ya suruali yake ya orange akagundua kuwa macho yamemponza, akarudi ndani.
Jumapili hiyo ilikuwa ni siku ya burudani na michezo huwa mara moja kwa miezi mitatu, Eman akaketi kwenye nyasi akiangalia wafungwa wenzake wakisakata kabumbu, kila alipoangalia huku na huku hakumuona Golam, alishindwa kujua kama Golam alikuwa mzuka au mfungwa mwenzake, mara akaanza kucheka mwenyewe alipokumbuka tabasamu la Golam. Aliondoka eneo hilo na kusogea pembeni huku akimuangalia kila anayekutana naye labda atamuona lakini hakufanikiwa, aliendelea kuvuta hatua taratibu akiwa bado na mawazo lukuki na maswali yasiyo na majibu.
Golam wa Golam, mfungwa asiyependa kuongea sana na anayependa kufanya kazi muda wote, alikuwa amepangwa kufanya kazi jikoni kama mpishi na kwa miaka miwili sasa. Golam alifungwa katika gereza la Sogera yapata miaka saba sasa kwa kosa la mauaji, alikuwa hapo akisubiri hukumu yake ya kunyongwa kwa kosa hilo. Alipokuwa gerezani humo hakupenda kujichanganya na wafungwa wengine hakuwa na rafiki na daima alionekana mtu mwenye kupanga kitu fulani, kwa kipindi cha miaka saba hii hata ndugu zake walishajua kuwa amenyongwa, hawakuja kumtazama wala kumtaka hali. Alipata kufahamu njia zote za gereza hilo na ratiba zote za askari za ulinzi wa gereza hilo. Aliwahi kuwa na rafiki mmoja tu ambaye yeye alishanyongwa pale tu alipojaribu kutoroka kwenye ngome hii isiyopenyeka.
Akiwa bize na kazi ya kuandaa chakula cha jioni cha siku hiyo Golam alionekana mtulivu sana hata alikuwa anafanya kazi dakika chache na chache anapumzika lakini akizama katika fikra zingine.
Eman alirudi kwenye kichumba chake na kujilaza kwenye kigodoro chake kidogo, baridi ilikuwa kali sana siku hiyo, akiwa amejilaza hapo alipitiwa na usingizi.
‘Watu warefu walikuja wakamkEman Eman, wakambeba juu juu, watu hao Eman hakuweza kuwaona miguu yao wala sura zao, walimpitisha kwenye bonde kubwa lenye manyoka makubwa mengine yana vichwa viwili, manyoka yale yalijaribu kumrukia lakini kutokana na urefu wa hao viumbe waliombeba hawakuweza kumfikia kabisa. Mara walifika eneo kubwa la wazi, pale aliona viumbe wenye vichwa vibaya na vipembe vilivyojinyonga kama vya kondoo, katikati yao kulikuwa na chungu kikubwa kinachotoa mvuke wa ajabu. Mara wale viumbe waliombeba walianza kuwa wafupi mpaka kufikia urefu wa wale wengine, walimpomshusha, Eman ndio aligundua kuwa wale viumbe wana miguu kama ya kuku na mikia pia walikuwa na jicho moja, wakamnyanyua ili kumtumbukiza ndani ya chungu, kumbe hawa viumbe wanakula watu baada tu ya kuwachemsha, Eman alipiga kelele za ajabu….’
***************
Mara alikurupuka kutoka usingizini kumbe alipitiwa na ndoto ya ajabu na mbaya. Jasho lilimvuja kama kamwagikiwa na maji, akitweta kama mtu aliyekimbia mbio fupi za mita mia moja. Alipotulia na kurudi katika hali ya kawaida huku akijiuliza maana ya ndoto hiyo aliona kipande cha karatasi chakavu chini ya mlango, alijinyanyua taratibu na kuokota kikaratasi kile, akakifungua kwa woga, kikaratasi kile kilikuwa kichafu lakini kwa taabu aliweza ona kilichoandikwa kwa muandiko ambao herufi zake ziko mbalimbali, alijaribu kuziangalia vizuri lakini ilimuia ngumu kuelewa ni nini kimeandikwa, alikiweka pembeni, alipoangalia nje kupitia kidirisha kidogo aliona bado ni usiku kwani ni mbala mwezi na nyota ndizo zilizong’aza nje, na mizunguko ya askari walio zamu kwa muda huo. Aliketi tena juu ya kigodolo chake akakunjua tena kijikaratasi kile, alipokigeuza kwa nyuma aliona mchoro wa ajabu, hakuweza kuuelewa mchoro huo, kitu chenye umbo la mraba, ndani yake kuna duara kubwa ambalo lililochorwa X, katikati ya x ile pamewekwa namba tano na mshale uliongalia juu, kabla ya kuishia mshale ule kamstari kengine kalikatisha na kufanya kitu kama mchoro wa dira katika kamstari kale kuliwekwa herufi A upande wa kulia na kuliandikwa lugha isiyoeleweka, Eman aliangalia mchoro ule akaona hamna anachokielewa akakunja kile kikaratasi tena akakiweka chini ya tandiko akajilaza. (insta - @kulayasimulizi )
Kulipopambazuka siku hiyo Eman aligubikwa na mawazo mengi alikuwa mpole sana kama mtu anayeumwa, siku hiyo alitakiwa kwenda na wafungwa wenzake kukata miti kwa ajili ya kuongeza idadi ya kuni kwa matumizi ya gereza. Wakiwa msituni na kazi imepamba moto, waliendelea na kuimba nyimbo mbalimbali za kuhamasishana huku wengine wakipakia magogo lorini, askari mmoja bwana mdogo alisogea karibu na Eman
“Mfungwa! Chagua wengine watatu tukashushe mzigo wengine endelea…”
alimwambia Eman. Wafungwa wanne wakapanda pamoja na Eman, akiwa amekaa juu kabisa ya lori lile pamoja na askari wawili wenye SMG wakiwa makini na kazi yao, lori lile aina ya Leyland lilikwenda kwa mwendo wa pole likiwa linapanda mlima mkubwa sana. Lilipofika juu ya mlima kabla alijaanza kuteremkia upande wa pili, Eman aligutushwa na mfungwa mwingine
“Eman! Cheki nyuma yako bondeni ilivo…”
alimwambia. Eman akaangalia kwa makini akaweza kuliona gereza ambalo wenyewe huliita nyumba, akaangalia vizuri, lilikuwa linaonekana bondeni hivyo aliweza kuliona vizuri sana. Mara akaona kitu cha ajabu kidogo aliweza kuiona vizuri picha ya gereza lile… aliliona katika mraba na alipokaza macho aliona kwa ndani kuna kama kitu cha duara kilichozunguka, Eman alishangaa sana akaingiza mkono kwenye nguo yake ya ndani akatoa kile kikaratasi mara akakumbuka kuwa alipo hapafai kufanya hivyo
“Mfungwa! Telemka huko kaa chini na wenzio!”
aling’aka kwa hasira akimnyooshea kiboko chake. Eman alishuka na kujichanganya na wengine.
Safari ilitimu wakashuka na kuanza kutelemsha kuni kupeleka jikoni, alipoingia jikoni alimuona Golam kwa mbali akiwa ametingwa na kazi. Golam nae akamuona Eman, akatoa lile tabasamu lake, Eman akamsogelea Golam
“Umeona mzigo wako?”
Golan alimuuliza Eman kwa sauti ya chini huku wakipanga kuni
“Mzigo gani?”
Eman akauliza
“Karatasi ndogo”
Golam akajibu
“Ndio! Ni nini kile? Sijaelewa”
Eman alimuuliza
“Mimi sijui! Nimepewa nikuletee”
alijibu Golam
“Oooh nani alikupa?”
Akauliza Eman
“Amesema utamkuta, muonane”
Golam alimueleza
“Nitamkuta wapi? Nani?”
Eman alizidi kuchanganyikiwa kabla hajauliza aliitwa na askari na wakaondoka.
Mvua kubwa ilinyesha jioni ile radi kali zenye ngurumo za ajabu zilendelea. Eman na wenzake walikuwa bado wapo kazini, sasa walikuwa wakirekebisha mitaro ya maji machafu , viatu walivyovaa vilikuwa vimelowa alkadhalika nguo zao zilikuwa chapachapa huku baridi kali ikiwapiga walifanya kazi chini ya uangalizi mkali tena wakati kama huu walifungwa minyororo miguuni. Baada ya kazi hiyo ilipigwa filimbi na wote walitakiwa kusimama katikati ya uwanja ule. Eman akiwa katikati kabisa ambapo nyuma yao kidogo kulikuwa ni sehemu ya kunyongea, mara akasikia sauti ya kitu kama jiwe liliodondokea batini upande wa kushoto akageuka upande ule, kulikuwa na kibanda kidogo kilichotumika kama choo kwa ajili ya askari, akufuatilia sana akageuka kuangalia mbele lakini kuna kitu kilimrudisha macho upande ule, katika mlango wa choo kile kulikuwa na mchoro wa pembetatu iliyojazwa rangi na katikati kulikuwa na duara ambalo halikupakwa rangi, mchoro ule ulimvutia Eman akakumbuka katika kile kijikaratasi upande wa nyuma kuna ule mchoro hapo akagundua lazima kuna siri ndani yake kwa nini michoro hii ifanane, hapo akavuta taswira akakumbuka jinsi alivyoona gereza lile kwa juu wakiwa juu ya mlima akaoanisha hivi vitu vitatu akagundua kuna siri ndani yake
‘labda Golam anafahamu siri hii’
alifikiria moyoni. Mvua kubwa iliendelea kunyesha
“Kutokana na hali ilivyo hatuwezi kuendelea na kazi”
aliwaambia askari mmoja, kisha akaendelea
“mtapanga foleni mtachukua chakula na kwenda kupumzika, hatakiwi mtu kuonekana nje!”
Wakiwa katika foleni ya chakula, Eman alikazia macho sana upande ule, alikuwa bado anatafiti kichwani mwake ni kwa nini michoro ile ilifanana na ile ya kwenye kijikaratsi kile kinachoonekana kuchakaa sana pia ni kipande tu je kingine chake kikowapi, alikosa jibu.
**************
Usiku ule tafrija ya maafande iliendelea, pombe za kufa mtu zilikuwa huko, Eman alikuwa ni mmoja wanaosaidia katika tafrija hiyo, lakini akili yake yote ilikuwa ni kuingia ndani ya choo kile aone tu kuna nini, kwa mbali alimuona Golam nae yuko bize kuhudumia katika meza ya wakubwa, brassband iliendelea kupiga mziki wa taratibu. Eman alijaribu kuangalia ulinzi uliopo muda huo aliona hakuna mabadiliko kabisa lakini alijaribu kutafuta nafasi japo aonane na Golam.
Alipokuwa stoo akipanga vinywaji kwenye chano mara Golam aliingia moja kwa moja akamfuata Eman
“Tutafute muda tukajisaidie!”
alimnong’oneza Eman. Eman akapokea kwa mshangao kauli hiyo lakini baadae akaona kuwa lazima Golam anafahamu chochote juu ya choo kile.
“Wakianza kuchangamka tu tuonane ili tujue tunaingiaje pale chooni, maana kwa nyuma kuna mlinzi na juu kabisa yupo mwingine na taa kubwa inamulika ule mlango”
Golam aliendelea kumdokezea Eman. Akili ya Eman ilianza kufanya kazi kwa kasi na shauku ya kuingia pale ilimjaa, lakini aliwaza
‘vipi wasipokuta chochote mle ndani na wakasthukiwa na askari, itakuwaje’
alikumbuka yule jamaa jinsi alivyonyongwa akaingiwa na woga. Lakini alijipa moyo na kuamua kutoa dozi ya pombe ili hawa jamaa wachangamke mapema.
Punde si punde, sherehe ilichangamka, watu waliimba na kucheza, Golam akazunguka upande wa Eman akampigia mbinja, Eman alipogeuka akamuona Golam, Golam akampa ishara ya mkono kuwa azunguke upande wa pili wa jengo hilo, alipofika upande huo alikuta miili miwili ya askari ikiwa chini, Golam akamwambia Eman avae uniform ya mmoja wao, akafanya hivyo japo nguo ile haikumkaa sawia lakini alionekana kama mmoja wa maafande, Golam naye akatwaa za yule mwingine halafu wakawavalisha nguo zile za ufungwa, Eman hakujivunga akabeba SMG na magazine mbili za akiba akamuoneshea alama ya dole gumba
“Naingia vitani!” (insta - @kulayasimulizi )
Eman alinong’ona kwa Golam. Golam aliondokea upande wa pili na Eman upande mwingine, kazi ikaanza.
Hadi kufika katika choo kile kutoka walipo akina Eman ni kama mita mia nne hivi na katikati hapo kuna mataa makubwa yanayoangaza hata akipita panya taa zile huzungushwa kufuatilia kinapoelekea kitu hiko, jinsi walinzi walivyo makini. Eman akajiweka tayari na kwa mwendo wa taratibu akiwa amejifunika koti lile la magereza, alivyojipapasa mfukoni alikuta kuna sigara alipoitoa aligundua kuwa ni msokoto wa bangi, Eman akatabasamu kwa sababu ana muda mrefu sana bila kupata hiyo kitu. Aliendelea kupita na kiambaza cha ukuta chini ya vibanda vya walinzi, alipofika upande ule ambako ndiko choo kile kilipo alitulia kidogo kwenye kona moja kwa kuwa aliona mtu akija upande ule aliokuwepo. Eman alisimama kikakamavu akiwa kampa mgongo mara alihisi kashikwa begani alipogeuka taratibu aligundua kuwa alikuwa Golam
“Shhhhhh!!!”
Golam alimuashiria Eman kutulia kisha akampita na kumpa ishara ya kumfuata, Eman alimfuata kwa nyuma wakazunguka nyuma ya jengo ambalo hutumika kama stoo ya kuni wakalipita na kuendelea mbele kisha Golam akasimama juu ya kitu kama tanki kubwa liliochimbiwa ardhini, akatoa katochi kadogo kama peni ambako alikakuta ndani yan nguo zile akamulika juu ya mfuniko wa tanki lile, kulikuwa na matenki kama matano. Eman hakuelewa Golam anaangalia nini juu ya matank hayo, tank la tatu akamwita Eman kisha akampa ishara ya mkono kumuonesha kwamba
‘ni hapa’,
Eman na Golam wakasaidiana kufungua mfuniko hule na walipofanikiwa Golam aliingia wa kwanza na Eman akafuatia kisha wakafunga mfuniko ule kwa ndani.
Ndani yake kulikua na shimo na kulikuwa na giza nene sana hata huwezi kuona kitu kilicho mita moja mbele yako, Eman alijaribu kukanyaga taratibu na Golam akafuatia, Golam akatoa katochi kake mfukoni na kuangaza kidogo, ni mwanga hafifu sana uliotoka katika tochi ile haikuweza kuangaza mbali, taratibu Eman alimfuata Golam alikoelekea kwa mwendo wa kunyata, ukimya uliokuwa ndani ya shimo lile ulitisha, kawa mwendo ule ule wakiangaziwa na mwanga hafifu, Eman aliogopa sana kutokana na giza lile alitamani kumwambia kitu Golam lakini alishindwa pia aliona labda akifanya hivyo ataaribu utaratibu asioujua, mara ghafla wakasikia kelele kama za mbawa za njiwa arukae kabla Eman hajajiweka tayari Popo mkubwa alipita usoni kwake na mbawa zake zikampiga usoni, Eman alitoa mguno wa sikitiko lakini hakuthubutu kupiga kelele alivumilia tu, bado waliendelea kupiga hatua ndogondogo. Baada ya kutembea kwa mwendo huo kama dakika kumi na tano hivi Golam akasimama ghafla kisha akamzuia Eman kwa mkono wake walisimama katika ukimya wa hali ya juu kama sekunde hamsini hivi. Eman alitamani kumuuliza kitu Golam lakini bado alishindwa ila alihisi kitu fulani kumkaba kooni kutaka kusema lakini aliona sio wakati muafaka japo alipenda kujua hata ni wapi wanaelekea.Walitembea taratibu mwendo kama wa lisaa limoja, masikio ya Eman yalikuwa kama yanataka kuziba kwa ukimya ule ambao hajawahi kuuhisi katika maisha yake, mara akaanza kusikia sauti kama za njiwa dume na jike wakiwa katika harakati za mapenzi na punde tu zikapotea akaanza kusikia sauti za mbu wengi sana wakitaka kuingia masikioni lakini alipopunga mkono wake upande wa sikio hakuhisi kugusa chochote akasikia kama wanamfuata kwa nyuma akageuka hakuona kitu huku akivuta hatua ndogondogo mara akahisi kugonga kitu alipotazama mbele alijikuta amegonga ukuta... hakuna njia... Golam haonekani! Matatizo.
Eman alipapasa ukuta ule akaona ulikuwa wa mawe makubwa ambayo si ya kujengwa na binadamu bali ni mwamba mkubwa, mkono wa mtu ukamshika begani Eman akashtuka na kupiga ukelele wa nguvu alipogeuka alimuona Golam,
“Usipige kelele !!”
Golam akamsisitiza Eman
“Utawaamsha mapema!”
Aliongeza Eman hakuelewa alichoambiwa na Golam
‘nani wataamka mapema?’
alijiuliza bila jibu Mbele kidogo walikuta kuna milango milango ipatayo kama nane hivi, Golam akasimama akatoa kipande cha karatasi kutoka kwenye nguo yake ya ndani akakimulika kwa mwanga hafifu wa kale katochi ambako tayari betri zake zilishaanza kupoteza nguvu. Golam akawa kama anahesabu kitu fulani katika ile milango kisha akampa ishara ya kumfuata Eman akafanya hivyo, walipita kwenye moja ya hiyo milango huko wakatembea kwa mwendo wa haraka kidogo, Eman aliendelea kusikia sauti za vitu mbalimbali mara watu wanacheka mara wanalia, kwake ilikuwa ni uoga mtupu. Mbele kidogo baada ya mwendo wa kama saa moja ingine Eman alianza kusikia kelele za maji mengi kama mto upitao, akamtazama Golam ambaye alikuwa amesimama kimya kama gogo, akamsogelea akamuona Golam kafumba macho katulia sana hakumshtua akasubiri aone nini kinafuata.
“Maji !” Golam alinong’ona na Eman akasikia mnong’ono huo
“Sasa tufanyeje?...”
Eman naye alijibu kwa swali kwa kunong’ona
“Lazima tuvuke, tufuate huu mto... mto Solondo”
Golam alimjibu Eman
“Mto Solando!?”
Eman alishangaa na kumuuliza Golam
“Ndiyo. Huu ni mto wa Solondo, lazima tuvuke kwa kuogelea kuna watu wanatusubiri nje, ila tahadhali mto huu una Mamba na maajabu mengi uwe makini, unajua kuogelea?”
Golam akamwambia Eman (insta - @kulayasimulizi )
“Najua kidogo sijawahi kuogelea kwenye maji mengi kama haya, hakika nitakufa.”
Eman alijibu kwa kuhuzunika
“Acha ujinga Eman! Ukisema utakufa, utakufa kweli”
Golam alimwambia Eman kwa ukali kidogo na kumtupia swali
“haya unajua haya maji yanaelekea upande gani?”
Eman kwa uoga akajibu
“Sijui mbona hata maji yenyewe siyaoni nasikia mvumo tu”
“Ukipiga hatua mbili utatumbukia mtoni. Niambie haya maji yanaelekea upande gani?
Tunatakiwa kuelekea upande yanakotoka siyo yanakokwenda...”
Golam aliendelea kumuambia Eman.
Golam akachuchumaa na Eman akafanya vivyo hivyo,
“Papasa kwa mkono polepole mpaka ufike ukingo wa mto kisha tumbukiza japo kidole uone maji yanaelekea wapi!”
Golam alimwambia Eman. Eman akafanya hivyo akapapasa na mara akahisi kafika mwisho wa kanjia kale na kelele za maji ziliongezeka, akaingiwa na woga mkuu, moyo wake ulikuwa unadunda kwa kasi na kijasho kumtiririka. Akayagusa yale maji yalikuwa ya moto kama yako jikoni akahisi mkono wake unavutwa upande wa kulia, akajaribu kuutoa alihisi kama kitu kimemshika mkono kinamvuta majini, nguvu zikamuishia akapiga kelele... Whatsapp +255 758 018 597

Post a Comment

0 Comments